Halloween party ideas 2015





Kuongezeko  kwa  makampuni  na  taasisi  mbalimbali   kumeleteleza  wingi  wa  ajira  maeneo  mbambali  ya  nchi.  Mbali  na kuongezeka  kwa  ajira  hizi  kumekuwepo  na tatizo  kubwa  la  waajiriwa  kutojua  haki  zao  mbalimbali  wawapo  maeneo  ya  kazi.  Niseme  jambo  moja  tu  kuwa  hakuna  suala  la msingi  kama   muajiriwa  kujua  haki  zake. Hii  ni  kwasababu  kupitia  kujua  haki  zake  ndipo  anapoweza kupata  ujira  stahiki, posho  stahiki, masurufu stahiki, mafao stahiki, malipo stahiki  ya  kuachishwa  kazi  ikiwa  ni  pamoja  na  ujumla  wa  kufanya  kazi  kwa  misingi  ya  kazi.  

Ni  muhimu  kila  mfanyakazi  kupitia pitia  haki  zake  mara  kwa  mara ili  kujua  nini  anapata  na  nini hapati. Uwe  kazini  au  umeachishwa  bado  ipo  nafasi  ya  kudai  haki  hizi  ili  upate kilicho  chako. Ukitegemea  mwajiri  ndio  akwambie  haki  zako  utakuwa  unajidanganya  kwasababu  yawezekana  kabisa  faida  kubwa ya  mwajiri  ipo  katika  wewe  kutokujua  haki  zako. Ni  hasara  kubwa  kufanya  kazi  bila  kujua   haki  zako . Kutokana  na  hilo  leo  nitaeleza   baadhi  ya  haki  za  mfanyakazi.

1.  HAKI  YA  KUJUA  SEHEMU  YA  KUFANYIA  KAZI.

Isiwe  uliambiwa  eneo  la  kazi  ni  Dar  es  salaam  halafu  ujikute  kila  siku  una  safari  za  mikoani  halafu  uambiwe  eti  hiyo  ndiyo  kazi  yenyewe,  hapana. Lazima  eneo  la  kufanyia  kazi  lijulikane  kwa  mfanyakazi.  Ijulikane  kuwa  umeajiriwa  na  eneo  lako  la  kazi  ni Dar  es salam , au  Mwanza au Kagera.  Hii  ina  maana  kubwa  kwakuwa  mfanyakazi  asipojua   eneo  lake  la  kazi  hataweza  kudai   malipo  yatokanayo  na  kufanya  kazi  nje  ya  ofisi .  Lakini  iwapo  unajua  eneo  lako  la  kazi  basi  utakapokuwa  nje  ya   eneo  la  kazi  yakupasa  kudai  malipo  ya  ziada. Kwa  hiyo  hakikisha  mwajiri  wako  unakuainishia  kwa  uwazi  kabisa  eneo  lako  la  kazi  na  ulijue. Nje  ya  hilo  eneo ni  malipo  mengine  ambayo  ni nje  ya  mshahara  wa  kawaida.

2.  HAKI  YA  KUJUA   MAHALI/SEHEMU  MWAJIRI  ALIPOKUTOA.

Waweza  kuwa  unakaa  Mwanza    lakini  mwajiri  amekuitia  kazi  Dar  es  salaam . Au  makazi  yako  ni  Arusha  lakini  kazi  iko  Mbeya. Mazingira  kama haya  yanazaa   haki  ya  msingi  unapokuwa  unaajiriwa.  Umuhimu  wake  ni  kuwa  wakati  wa  kustaafu  au  kumaliza  mkataba  au  ikitokea  umeachishwa  kazi  basi  ni  wajibu  wa  mwajiri  kuhakikisha  anakusafirisha  kutoka   eneo  la  kazi  mpaka  alipokutoa. Anatakiwa  kukusafirisha  kwa  kutoa  usafiri  au  kutoa  gharama  za usafiri  ukasafiri  mwenyewe.  Hautoweza  kupata  haki  hii  iwapo   hujui  kitu  kama  hiki.

3.  HAKI   YA  KUJUA  AINA  YA  KAZI  UNAYOTAKIWA  KUFANYA.

Lazima  kazi  unayotakiwa  kufanya  ijulikane  vyema. Isiwe  unafanya  kila  kazi  inayokuja  mbele yako. Mchanganuo  wa  kazi  uwe  wazi. Kama  ni   sekretari  ijulikane  kazi  ni  zipi  na zipi. Kama  ni  meneja  ijulikane  kazi  ni  zipi  na  zipi  kwa  mchanganuo  wenye  kueleweka  kabisa. Hii  husaidia  kutofanya  kazi  ambazo  si  zako  au  kufanya  kazi  nje  ya  makubaliano. Kwa  kujua  haki  hii  kazi  yoyote  utakayopewa  iliyo   nje  ya  mchanganuo  wa  kazi  zako, utapatana  upya  na  malipo  yake  yatatakiwa  kuwa  nje  ya  mshahara.

4.HAKI  YA  KUJUA  MCHANGANUO  WA MSHAHARA.

Mshahara  ni  jambo  moja  lakini  mchanganuo  wa  mshahara  huo  ni  kitu  kingine.  Mwajiri  anaweza  kukwambia  mshahara  ni  laki  saba . Swali  ni  je  laki  hiyo  saba   inagawika  vipi.  Ili  uendane  vizuri  na  haki  hii  mara  nyingi  usiiangalie  ile  laki  saba  isipokuwa angalia  mchanganuo  wa  laki  saba.  Lazima  mwajiri  aoneshe  kati  ya  hiyo  laki  saba  mshahara  kamili( basic  salary)   ni  upi, kodi  itakuwa  kiasi  gani, posho  ya  usafiri  itakuwa  kiasi  gani, posho  ya  chakula  itakuwa  kiasi  gani,  posho  ya  pango  la  nyumba  ya  mfanyakazi  itakuwa  kiasi  gani,  fedha  za mfuko  wa  hifadhi  ya  jamii  kiasi  gani,  na  makato  mengine  yote  ambayo  hutokana  na  makubaliano  kati  ya  mwajiri    na  mwajiriwa  yajulikane  vyema.  Hii  husaidia  hata  kudai malimbikizo  kwa  usahihi   baada  ya  kazi  kuisha. Huwezi  kupata  stahiki   zako kwa  kiwango  unachotakiwa  kulipwa  hasa  baada  ya  kazi  kuisha kama  huyajui  haya.

5.HAKI  YA  KUJUA  AINA  YA  MKATABA  WA  KAZI.

Wapo  watu  ambao  wako  makazini  na hela  wanapata  na  maisha  yanakwenda  lakini  hawajui  wanafanya  kazi  kwa  mkataba  wa aina  gani.  Ni  hatari  kutojua  aina  yako  ya  mkataba  kwakuwa  utalazimika kukosa  baadhi  ya  haki  zinazotokana  na  mkataba  wako  yakiwemo  malipo  na  posho nyinginezo. Lazima  ujue  kama  mkataba  wako   ni wa  muda  au  wa  kudumu. Mkataba  wa  muda  unao  masurufu  yake  na  wa  kudumu  unao  masurufu  yake. Usipolijua  hilo  utayakosa  hayo  masurufu.  Mkataba  wa  muda wa  ajira  ni  ule  ambao  ni  wa kipindi  fulani  kwa  mfano  mwaka  mmoja  lakini  waweza  kuongeza au  miaka  miwili n.k. Kwa  hiyo  ni  vyema  upitie  mkataba  wako wa  ajira  ili ujue  ni  wa  aina  ipi.

6. HAKI  YA  KUJUA  KAMA  KUNA  KIPINDI  CHA  MPITO.

Kipindi  cha  mpito  hujulikana  kama probation  period.  Hiki  ni  kipindi  ambacho  unakuwa  umeajiriwa  lakini  ukiwa  chini  ya  uangalizi  maalum  wa  kupima  ufanisi  wako  katika  kazi. Ni  muhimu  kuwekwa  wazi  kipindi  hiki  kitaanza  lini  na  kuisha  lini na  ni  haki  zipi ulizonazo  ndani  ya  kipindi  hicho. Nasema hivyo  kwakuwa  wapo  watu  ambao  wamewekwa  katika  kipindi  hiki  kwa  miaka  mingi  tu huku  wakikosa  stahiki  kamili  za  ajira  na  pia wakikosa  hata  stahiki   za  hicho  kipindi. Hii  si  sawa  na  hulenga  kumminya  mfanyakazi  na  kumfaidisha  mwajiri.  Hivyo  ni  muhimu  uambiwe  kipindi  hiki  kinaanza  lini  na  kinaisha  lini  na una  haki  gani  ndani  ya  kipindi  hicho.




You may contact us through

Email : lawyersheria@gmail.com

 phone number: +255 620 212 960










Wakati  mwingine  kujilinda  waweza  kukuita  kujitetea,kujiokoa au kujikinga.  Ni  hali  ambapo  mtu  hufanya  jitihada  za  kujinasua  katika  tendo  ovu  ambalo  linatekekezwa na  mtu  mwingine  dhidi  yake.  

Mfano  wake  ni  kama  kuvamiwa  na  majambazi, kutekwa, kufanyiwa  fujo  ya  aina  yoyote, kupigwa au  kujaribu  kupigwa n.k. Matukio ya  namna  hii  au  yanayofanana  na  haya ni  sehemu  yetu  ya  maisha.  Yumkini  yanapotutokea  huw  tunachukua  hatua.  Na moja  ya  hatua    ya  awali  kabisa  tunayochukua  huwa  ni  kujaribu  kujitetea   au  kujikinga  nayo .

Umevamiwa  nyumbani   na  majambazi,  umefanyiwa  fujo  njiani  kwasabasbu  yoyote  ile  na  wewe  unaamua  kujitetea  ili  usidhurike,  na  katika  kujitetea  huko   unasababisha  kifo  cha  mtu, awe  yule aliyetaka  kufanya  fujo au mwingine  mpita  njia.  Sheria  inasemaje  kuhusu  mkasa  wa  aina  hii.  Makala  yataeleza  japo  mambo  ya  msingi  kuhusu  hali hii.

1.HAKI  YA  KUJILINDA.

Haki  ya  kujilinda  ni  haki  ya  kisheria. Ni  haki  ambayo  ipo  kwa  kila  mtu.  Mbali  na  kuwa  haki  hii  ni ya  kisheria  pia  haki hii ni  ya  kuzaliwa. Kuna  tofauti  kati  ya  haki  kuwa  kisheria  na  kuwa  ya  kuzaliwa.

Haki  za  kisheria  ni  zile  haki  zote  ambazo  zimeelezwa  ndani  ya  sheria.  Zimekuwepo  baada  ya sheria  kutungwa na  hivyo  kabla  ya  sheria  kutungwa  hazikuwepo. Haki  ya  kuzaliwa  ni  haki  ambayo  imekuwepo  tangu  mwanadamu  wa  kwanza  alipokuwepo.  Ni  haki  ambayo  mtu  anazaliwa  nayo.

Haki  hii  haihitaji  kuwa  ndani  ya  sheria  ili  mtu  awe  nayo  isipokuwa  tu  anapozaliwa  nayo  huzaliwa. Hukua  nayo  na  hufa  nayo. Kujilinda  au  kujitetea  pale  mtu  anapotaka  kukudhulu hakuihitaji  kuwa  ndani  ya  sheria  ili ndo  umzuie asikudhulu.  Isipokuwa  ni  jambo ambalo  hutokea  lenyewe(automatic).Lipo  tu hata sheria isiliseme.   

Kwahiyo pamoja na  kuwa haki  ya  kujilinda  usidhurike  ni  haki  ya  kisheria  lakini  kubwa  zaidi  ni kuwa  haki  hii  ni  haki  ya  kuzaliwa. 
Haki  nyingine  za  kuzaliwa  ni  kama  haki  ya  kuishi, ukishazaliwa haki  ya  kuishi  inakuwepo sio  mpaka  iwe  kwenye  sheria, haki  ya  kuzungumza, ikiwa  umezaliwa  unazungumza  basi  hiyo  ni  haki  ambayo  husubiri  sheria  iitoe, haki  ya  kutembea n.k.  Haki  ambazo  si  za  kuzaliwa  ni  kama  hizo  za kuchagua  au  kuchaguliwa,  kupiga  kura, haki  elimu n.k.

2.   UNAPOSABABISHA  KIFO  UKIJARIBU  KUJILINDA/KUJITETEA.

Kifungu  cha  18 cha  Kanuni  za  adhabu , sura  ya  16 kinasema  kuwa   mtu  hawezi  kuwajibika  kijinai  kwa  kitendo  alichokifanya  wakati  wa  kutimiza  haki  yake  ya  kujitetea, kumtetea  mtu  mwingine,  au  kutetea  mali.

Kifungu  hiki  kinasomwa  na  kifungu  cha  18c kinachosema  kuwa  haki  ya  kujilinda, kumlinda  mtu  mwingine au  mali itatumika  kwa  mtu  yeyote  ambaye  katika  kutumia  haki  hiyo  atasababisha  kifo  au  dhara  kubwa  kwa  mtu  mwingine.

Maana  ya  vifungu  hivi  ni  kuwa  haki  ya kujilinda  itatumika  kama  kinga  kukuondolea  hatia  ya  jinai  iwapo  umesababisha  kifo. Lakini  ili  ikubalike  kama  kinga  na  usitiwe  hatiani  kwa  kosa  la  kuua  vifungu  hivi  vimetoa  masharti  yafuatayo.

( a ) Kwanza  wewe  uliyesababisha  kifo  uwe  umesababisha  kifo  hicho  kwa  nia  njema  kwa  maana  ya  kuwa  ulikuwa  kweli  kabisa  ukijilinda  usidhulike. Isije  kuwa  unatumia  nafasi  ya  kujilinda  kumuua  au  kumdhulu  mtu  mwingine   kwa  makusudi  ukijifanya  ulikuwa  ukijilinda. Swali  la  ulifanya  makusudi  au  kwa  nia  njema ya  kujilinda  litathibitishwa  kitaalam  na  mazingira  ya  tukio husika.

( b ) Kitendo  ulichofanyiwa  kiwe  ni  kitendo  ambacho  kiukweli  ulitakiwa  kutumia  nguvu  kiasi  cha  kusababisha  kifo.  Isiwe  mnatupiana  maneno  mawili matatu halafu unasababisha  kifo  kwa  kisingizio  kuwa  ulikuwa  ukijilinda  usidhulike. Kuwe  na  mazingira  ambayo hata  ukiyatizama  yafanane  na  hatua  ya  kujikinga  hadi  kusababisha  kifo.

( c )  Pia  ikiwa  kitendo  kinahusu  kubaka  au kufanya  kinyume  na  maumbile  kinga  ya  kujikinga  hadi  kusababisha  kifo inaswihi.

( d ) Pia  kujikinga/kujitetea  hadi  kusababisha  kifo  kunakubalika  ikiwa  tendo  linahusisha  kuteka  nyara,  au  kutorosha.

( e ) Pia  matendo  kama  kuvunja  na  kuingia, unyanganyi, kuchoma  moto,  nayo  yanakubalika   katika  kujikinga  hadi  kusababisha  kifo.


Kwa  kumalizia  zingatieni  kuwa  ikiwa  upo  katika  mazingira  ambayo  unaweza  kujikinga/kujitetea  bila  kusababisha  kifo  au  madhara  makubwa  basi  ni  vema  kufanya  hivyo. Kujikinga  hadi  kuua  liwe  chaguo  la  mwisho  pale  unapokuwa  huna  namna  nyingine  yoyote  isipokuwa  kufanya  hivyo. 

You may contact us through

Email : lawyersheria@gmail.com  

 phone number: +255 620 212 960

Upo wakati kwenye  ndoa ambapo mmoja  wanandoa  anaweza akawa anataka  kuuza au kubadili jina la nyumba/kiwanja  bila ridhaa ya mwenzake ilihali  nyumba  hiyo  ni ya  familia. Lakini  pia  nje ya  hilo kuna  mazingira  ambayo  mtu anaweza  kuwa  si  mwanandoa lakini ana maslahi  katika  nyumba au  kiwanja cha mtu fulani  na anataka  kuzuia  nyumba/ kiwanja  hicho  kisibadilishwe  jina au kisiuzwe.  Kisheria jambo hilo linaruhusiwa  na huitwa zuio( Caveat).

Hili sio zuio la kwenda mahakamani  kama  mazuio tuliyoyazoea.Hili  ni zuio jingine  kama  nitakavyolieleza. Aidha  kuzuia hati  isibadilishwe  kimsingi ni sawa na  kuzuia nyumba isiuzwe.  Hii ni kwakuwa  hakuna namna ambavyo  mnunuzi anaweza kununua  kitu ambacho  hakiwezi  kubadilika  na kuingia  katika  jina  lake. Ikiwa  mke ana wasiwasi kuwa mume  anaweza kumzunguka  na kuuza mali ya familia  au mume ana wasi wasi juu ya uwezekano  wa mke kuuza basi wanayo  ruhusa  ya kuweka zuio ili hati  ya  nyumba  isibadilishwe.  Yapo mambo mengi kuhusu hili nitaeleza baadhi.
      
  1.         NINI  MAANA  YA  ZUIO.

Zuio ni usitishwaji wa muda ambao huwekwa ili kuzuia mabadiliko yoyote katika hati. Kama maana  yenyewe inavyojieleza  huu unakuwa ni usitishwaji wa muda  ambao unalenga  kulinda  maslahi ya  mtu aliyeomba  zuio.Kuitwa  zuio  la  muda haimaanishi  kuwa  mtu akizuia   itakuwa  ni mwezi mmoja  au  miwili basi, hapana. Ni  zuio  la  muda  kwakuwa  haliwezi kukaa milele  lakini  mtu akishaliweka  linaweza  kukaa  hata  miaka  mingi  kutegemea  na  sababu  za  zuio  hilo.

      2.      MWANANDOA   KUZUIA   HATI  ISIBADILISHWE.

Lazima  ieleweke  wazi kuwa si  kila  mtu anaweza  kuamua  na akazuia   hati  ya mtu isibadilishwe  . Wapo watu ambao  kwa mujibu  wa  sheria  wanayo  haki  ya  kuomba  hati  isibadilishwe.  Kwanza mke au mume  mmoja  kati  yao anaweza  kuweka  kizuizi katika nyumba ya ndoa (matrimonial  home) iwapo kuna  dalili  kuwa mmiliki aliyeandikishwa  anaweza kuiuza au  kuiweka  rehani  bila ya ridhaa ya mwingine. Mara  nyingi  migongano  katika  familia  inapoanza  mmoja  kati  ya wanandoa  hukimbilia  kuuza  baadhi  ya  mali  kwa aidha kumkomoa  mwenzake au  sababu nyingine yoyote.  Kwa hiyo  ili kuliepuka  hilo unapogundua  kuwa  kuna  uwezekano  huo  basi  sheria  imekuruhusu  mwanandoa  kuweka  zuio  ili  hati  isibadilishwe  na hivyo  kuepuka kuuzwa kwa  mali.

3. HATA  MKOPESHAJI   NAYE  ANAWEZA  KUWEKA   ZUIO KWENYE   HATI   YAKO.

Nimezungumzia  zaidi  wanandoa  kuzuia   lakini  pia  ieleweke  wazi kuwa suala  la  kuzuia  si  tu la wanandoa. Kampuni, shirika, mtu  binafsi au taasisi  ya  fedha  iwapo imemkopa  mtu  na  akaweka  nyumba/kiwanja  kama  dhamana  ambacho  kina  hati basi  wanayo  ruhusa  ya  kisheria  ya  kuomba  zuio  liwekwe  kwenye   hati ile  ili dhamana  isije kutumiwa  kukopea  pesa  katika  taasisi  nyingine  au  kuuzwa  wakati ipo  kulinda  deni. Kwa hiyo  iwapo  mtu ana  maslahi ya  namna  hii kwenye  ardhi  inayomilikiwa  na mwingine  basi  ni haki  kwake  kuweka  zuio hili  ili  kulinda  maslahi  yake.

4. WAPI UPELEKE MAOMBI YA KUZUIA  HATI           ISIBADILISHWE.

Mamlaka  za ardhi  ni mamlaka  ambazo  hutakiwa  kupelekewa  maombi  haya  ya  zuio.  Mara nyingi  mamlaka  za ardhi  huwa zipo  katika  ofisi  za wilaya  au  manispaa katika mkoa wako isipokuwa  kwa walio  Dar  es salaam  maombi  hupelekwa   makao  makuu  pale  wizara  ya ardhi  kama  ni hati.

5. MAOMBI YA KUZUIA HATI ISIBADILISHWE         HUANDALIWAJE.

Maombi  haya  si  maombi  kama  maombi  mengine  yalivyo. Maombi  haya  ni maombi  ya  kisheria  na  huandaliwa   katika  ofisi  za wanasheria   na  hupelekwa  yakiwa  na  muhuri  wa mwanasheria. Karika  maombi  hayo  mwombaji  hueleza  jina  lake  kwa urefu, anuani  yake,  uhusiano  wake  na  yule ambaye  jina  lake  ndilo  liko kwenye  hati yaani anayemwekea zuio   huku  akieleza  sababu  za  msingi  kwanini   anataka  kuzuia  hati  isibadilishwe.

6.  LAZIMA  MAOMBI  YAAMBATANE  NA  NYARAKA  HIZI.

Kwanza,  picha  2  za mwombaji  huku kila picha  moja  ikibandikwa kwenye  nyaraka  moja.

Pili, risiti  za malipo ya ada ya usajili. Maombi  haya hulipiwa  kiasi  cha  fedha lakini si kikubwa sana kwahiyo  lazima uambatanishe  na risiti  za malipo.

Tatu, mwombaji aambatanishe vielelezo vinavyompa haki juu ya kiwanja husika kwa  mfano  cheti  cha  ndoa, mkataba  wa mkopo n.k.

Transfer  ni  kubadilisha  hati  au  leseni  ya  makazi  kutoka  jina  la  mmiliki  wa awali  kwenda  kwa  mmiliki  mpya.  Transfer  inaweza  kufanyika  kutokana na mauzo, kupewa  zawadi, fidia, n.k.  Kwahiyo  kuzuia  transfer  ni  kuzuia   kubadilishwa  kwa  hati  kutoka  mmiliki wa  awali  kwenda  mmiliki  mpya. Mara   nyingi  tumezoea   kuzuia   transfer  kwa  kutumia  mahakama ( court  injuction).

Sasa  yatupasa tufahamu kuwa  ipo  njia nyingine  nyepesi  ambayo  haihusishi  mahakama.  Ni  njia  ya  maombi  kwa  kamishna  wa  ardhi   kwa  mujibu  wa  Sura  ya  113 ,  sheria  ya ardhi ,namba  4, ya mwaka  1999  vifungu  vya  38, 39  na  41 . 

Kabla  ya kuona  ufanyeje  kutumia  njia  hii ni  vema  tuone    mazingira  ambayo   yakikutokea unaweza  kutumia  hiyo  njia.

1.HAYA  YAKITOKEA  UNAWEZA  KUPELEKA  MAOMBI  KWA  KAMISHNA.

( a ) Mme  wako  au  mke  wako  ameuza   kiwanja  au  nyumba  yenu  na  kuna  namna  ambavyo  mauzo  hayo   unadhani  sio  halali  kwasababu  yoyote  ile  ya  kisheria pengine ya  kutokushirikishwa,  au  kushirikishwa  lakini  baadae  kunyimwa  haki  yako  kwa  mujibu  wa  makubaliano au  vinginevyo. Lakini   wakati  huo   unadhani  huna  la  kufanya  kwakuwa  mauzo  tayari  yamefanyika  na  pengine  hata  wewe  ulishasaini.

( b ) Una  maslahi  na  haki  katika nyumba/kiwanja  cha  mirathi .  Mali  hiyo  imeuzwa  bila  wewe  kushirikishwa  au  umeshirikishwa  lakini  haki  zako  za  msingi  hazikuzingatiwa  au  namna  nyingine  yoyote  ambayo  kwayo  unahisi  mchakato  haukwenda  sawa.  Lakini   wakati  huo   unadhani  huna  la  kufanya kwakuwa  mauzo  tayari  yamefanyika  na  pengine  hata  wewe  ulishasaini.

( c ) Umemuuzia  mtu  nyumba/kiwanja  lakini  amekataa  kutekeleza  baadhi  ya  makubaliano  ya  msingi yaliyo  katika  mkataba  wenu  wa  mauziano  na  sasa  anafanya  mchakato  wa  kubadili  hati.

( d ) Na mazingira  mengine  yoyote ambayo  tayari  nyumba/kiwanja  kimeuzwa  lakini  ukaona  kuna  haja  ya  kuzuia  mchakato  wa  kubadilishwa jina  la  mmiliki  ili  baadhi  ya mambo yawekwe  sawa  kwanza.

2.   MAOMBI  KWA  KAMISHNA.

( a )Utaandaa  maombi  maalum  kwa  njia  ya  maandishi.  Maombi  utayaelekeza ( adress)  kwa  kamishna  wa  ardhi  Tanzania.

( b )Kichwa  cha  maombi  kitakuwa  kuzuia  kubadilishwa  kwa  umiliki  wa  nyumba/kiwanja  namba…,plot  namba….,  title  namba…… Utaweka  taarifa  zote  kama  zinavyoonekana  kwenye  hati.

( c ) Utaeleza  jina  lako  na  wewe  ni  nani  mpaka  utake  kuzuia  ubadilishaji  wa  umiliki.

( d ) Utaeleza  maslahi  yako  katika  nyumba/kiwanja  hicho  kwa  mfano  mke  halali, mkopeshaji, mrithi  halali,  mtia  sahihi  katika  mkataba  wa  mauziano,n.k.

( e ) Hakikisha  unaambatanisha  nyaraka  zote  muhimu  kama  kopi  ya  hati  kama  unayo, cheti  cha  ndoa, mkataba  wa  mkopo, mkataba  wa  mauziano  kama  unao, hati  ya  usimamizi  wa  mirathi n.k.

( f ) Utaeleza  ni  kwa  vipi  utaathirika  ikiwa  zuio  lako  halitakubalika  na  hivyo  transfer  kuendelea  na  hatimaye  kuhamia  jina  la  mmiliki  mpya.

( g ) Utaandika  jina  lako  na  utasaini,  kisha  utakwenda  ofisi  za  ardhi  na  kuuliza ofisi  ya  kamishna  wa  ardhi  ilipo  na  hapo  utaacha maombi  yako.

( h ) Pia wakati  mwingine kutokana  na  uharaka  wa  jambo   ni  muhimu  kuhakikisha unamuona  kamishna  wa ardhi na  kumueleza  tatizo  lako moja  kwa  moja.

3. FAIDA    ZA   NJIA   HII  DHIDI    YA  ILE  YA  MAHAKAMA.    

Haina  gharama  kubwa ,  ni  nyepesi,  haichukui  mda  mrefu, hatua  na  mchakato  wake  ni  za  kueleweka  zaidi, kwa  ufupi  njia  hii  ni  bora  zaidi  kuliko  ile  ya  mahakama.

Sheria ni nini?
Sheria ni masharti yanayowekwa katika nchi ili kutoa mwongozo wa jinsi ya kufanya mambo kwa usahihi. Sheria lazima zifuatwe na watu wote, na anayevunja sheria huadhibiwa.
Kanuni ni nini?
Kanuni ni maagizo kwa ajili ya asasi kubwa ya umma, zinazoongoza kufanya mambo yaliyo sahihi. Kanuni hizi mara nyingi zinafafanua sheria za nchi.
Taratibu ni nini?
Taratibu ni maelekezo yanayotolewa kwa idara zote za serikali ili kuelekeza kufanya mambo yaliyo sahihi.
1. Mwalimu ni nani katika mazingira yetu ya Tanzania?
Neno “mwalimu” limetafsiriwa kwenye ‘Kamusi ya Kiswahili Sanifu’ TUKI (1981) kwenye ukurasa wa 201 kuwa ni “mtu afundishaye elimu au maarifa Fulani, au mtu anayeonesha wengine”.
Katika Sheria ya Elimu, (sura ya 353 R.E.2002), neon ‘mwalimu’ limepewa maana kwenye fungu la 2 (1) kuwa ni “mtu yeyote aliyesajiliwa kama mwalimu chini ya sheria hii.”
Na fungu la (46) la sheria hii, linaonesha kuwa baada ya mtu kusajiliwa na Kamishna wa Elimu na kupewa cheti, basi mtu huyo anakuwa mwalimu.
2. Umuhimu wa mwalimu kufahamu sheria
Ili mwalimu aweze kutekeleza kwa ufanisi wajibu wake mbele ya umma anapaswa awe na sheria na miongozo ambayo itamsaidia kuelewa vyema utumishi wake kama mtumishi wa umma.
Kanuni za Mpango wa Utumishi wa Umma za mwaka 2005, zilizotolewa kwenye Gazeti la Serikali namba 331 la tarehe 28/10/2005 ambazo zinahusu watumishi wa umma wakiwemo na walimu zinaonesha nyaraka za sheria ambazo mtumishi wa umma anapaswa kuwa nazo.
Kanuni ya 31 (1) ya kanuni hizo inaorodhesha nyaraka hizo kuwa ni;
  1.  Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, (sura ya 2 R.E. 2002)
  2. Sheria ya Utumishi wa Umma (sura ya 298 R.E. 2002)
  3. Sheria ya Huduma ya Mafao ya Kustaafu (sura ya 371 R.E. 2002
  4. Sheria ya Mafao ya Kustaafu ya Viongozi wa Kisiasa (sura ya 225 R.E.2002)
  5. Sheria ya Huduma ya Umma (chombo cha upatanishi)
  6. Sheria ya Uajiri na Uhusiano wa Kazi (sura ya 366)
  7. Sheria ya Wakala wa Serikali (sura ya 245 R.E. 2002)
  8. Sheria ya Utawala wa Mkoa (sura ya 97 R.E. 2002)
  9. Sheria ya Taasisi za Kazi (sura ya 300)
  10. Kanuni za Utumishi wa Umma za Mwaka 2003
  11. Kanuni za Maadili na Tabia za Watumishi wa umma,
  12.  Kanuni mbalimbali za maadili na mwenendo wa wataalam
  13. Kanuni za Serikali kwa ajili ya huduma za Umma
  14. Kanuni za kuajiri wahudumu wa umma
  15. Kanuni za nidhamu ya wahudumu wa umma
  16. Kanuni ya usuluhishi na mapatano ya huduma ya umma
  17. Kanuni za kustaafu na kuachishwa kazi ya huduma ya umma
  18. Kanuni ya sera ya uongozi na uajiri wa huduma ya umma
  19. Sheria nyingine za nyaraka zinazohusika kwa ajili ya marejeo yanayohusika
3. Je, mtumishi wa kawaida anaweza kuzipata wapi hizi sheria na nyaraka anazopaswa kuwa nazo mtumishi wa umma?
Kwa mujibu wa kanuni ya 31 (2) na (3) ya Kanuni za Mpango wa Utumishi wa Umma za mwaka 2005 zinaeleza kuwa, “Kila mwajiri atapaswa kuhakikisha upatikanaji na fursa ya kutumia nyaraka zote anazopaswa kuwa nazo mtumishi aliye chini yake”.
SIKU hizi haipiti dakika hujasikia haki zikidaiwa mahali. Kuna haki za watoto. Haki za akina mama. Haki za wafanyakazi wa ndani(Koero analizungumzia hili vizuri). Haki za masikini. Haki za vyangudoa. Haki za maalbino. Haki za wasomaji. Haki za mafisadi (hata fisadi naye ana haki ya kusikilizwa/natural justice). Haki. Haki. Haki. Orodha ni ndefu.

Jambo moja. Inapodaiwa haki, ikumbukwe kuwa upo upande ambao utalazimika kunyang'anywa haki zake ili haki ile ya kwanza inayodaiwa ipatikane. Kwa maneno mengine, unajikuta ili kutetea haki, inabidi unyang'anye haki. Na upande huu wa pili unaolazimika kupoteza haki ili kufidia haki inayodaiwa, nao ukiamka, inabidi zoezi liwe mduara. Yaani poteza haki, kuleta haki.

Kwa mfano. Mtoto anapodai haki, maana yake inamlazimu mzazi kupoteza haki zake ili kumpatia mwanae haki. Kwa maneno mengine, haki ya mtoto inakuwa utumwa kwa mzazi. Unapoteza haki kuleta haki.

Mwanafunzi wa kike anapodai haki ya kusoma kwa upendeleo, inabidi mamlaka zinazohusika kubinya haki za wavulana ili haki hiyo inayodaiwa itimie. Hapa, maana yake unapoteza haki ili kuleta haki.

Sasa hapa ndiko liliko swali langu: Haki ni nini?

Na haki hizi ni kwa ajili ya nani, jamii, kikundi cha watu fulani wanaodai rehema ama ni mtu binafsi?

Inakuwaje kama tukiamua kuzivunja haki hizi? Je, haki ni kutii sheria na taratibu zilizopo kwa lengo tu la kuepuka adhabu?

Je, haki ni kile kinachoweza kufanywa na watu wengine ili kutupa faida hata kama kufanya hivyo kunawaumiza wao? (Je, wao hawana haki?)

Je, haki ni kuwa mtu mzuri anayekubalika kwenye jamii? (Vipi kama nikiamua kutafuta haki zangu kwa namna ninayoijua mimi hata kama kwa kufanya hivyo ntaonekana kituko?)

Je, haki ni kutimiza matakwa ya sheria zilizopo hata kama zinaingilia uhuru wangu?

Je, haki ni kutetea matakwa ya wengine, hata kama kufanya hivyo kunakunyima vitu fulani fulani
Je, haki ni matakwa ya kibinafsi yasilazimika kushahibiana na sheria zinazoonekna ni halali katika jamii?

Kumbuka palipo na haki kuna haramu. Pasipo tafsiri nzuri ya haki, tunajikuta kila tunalolifanya ni haramu. Mzunguko wa madai usioisha. Kupoteza haki. Kupata haki. Kupoteza tena. Kuzipata tena. Mwishowe, kila kitu kinakuwa haramu
Powered by Blogger.